Asimulia baba yake alivyotekwa na watu wenye silaha

By Jenifer Gilla , Nipashe
Published at 09:38 AM Apr 30 2024
Yusuph Mdoe.
picha: mwandishi wetu
Yusuph Mdoe.

WATU wasiojulikana wakiwa na silaha, wanadaiwa kumteka Yusuph Mdoe, mkazi wa Mbagala akiwa nyumbani kwake usiku wa Aprili 9, mwaka huu na mpaka sasa hajulikani alipo.

Mtoto wa kiume wa Mdoe mwenye umri wa miaka minane (jina linahifadhiwa), amesimulia jinsi watu hao walivyofika nyumbani kwao na kumchukua baba yake.

Amesema siku ya tukio, wanaume wawili walikwenda nyumbani kwao na kugonga mlango na alipowafungulia, walimtaka awaitie baba yake.

 Amesema alikwenda kumwita baba yake na alipofika mlangoni watu hao walimwelekeza awafuate nje kwa madai kuwa wana mazungumzo naye.

Mtoto huyo alisema baba yake aliwafuata nje watu hao waliokuwa na silaha kama walivyomtaka afanye.

 Amesema baada ya kutembea hatua kadhaa kutoka katika nyumba hiyo, watu wengine wanane walitokea na kuwafuata nyuma wakiwa pia wameshika silaha.

Mtoto huyo amesema walitembea mpaka yalipokuwa magari yao na kumpakiza ndani kisha kuondoka naye, na kwamba tangu siku hiyo hajarudi nyumbani wala hawajapata taarifa yoyote ya mahali alipo.

Baba mdogo wa Yusuph, Ally Abdallah ameiambia Nipashe kuwa, wameshatoa taarifa ya kutekwa kwa ndugu yao baada ya kumtafuta kwa muda mrefu bila mafanikio wakishirikiana na majirani.

 Amesema taarifa hiyo wameitoa Kituo cha Polisi Mbagala Maturubai na kupewa RB yenye namba MBL/RB/2891/2024.

 Amesema kijana wake hakuwa na ugomvi na mtu yeyote mtaani kwao na mke wake alimwaambia kuwa hajawahi kusikia wala kumhadithia kuwa ana uhasama na mtu yeyote nyumbani au kazini.

“Yusuph pia alikuwa anafanya kazi katika benki ya Habib iliyopo Stesheni jijini Dar es Salaam na wafanyakazi wenzake wametuhakikishia kuwa hakuwa na shida yoyote ofisini na tunashirikiana nao kumtafuta,” amesema.

 Amesema yeyote atakayemuona ndugu yao atoe taarifa katika Kituo cha Polisi cha Mbagala Maturubai au kilichopo karibu naye au apige simu namba 0676125590 au 0717699898.