WAZIRI wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Jerry Silaa amezindua mradi wa nyumba za gharama nafuu eneo la Morocco jijini Dar es Salaam wenye lengo la kuwapatia makazi wakazi wa Jiji la Dar es Salaam.
Mradi huo unatekelezwa kwa ushirikiano na makampuni mawili ya mawili ya RE/MAX Coastal and Coral Property umelenga kuunga mkono juhudi za serikali kuhakikisha makazi ya wananchi yanaboreshwa.
Akizungumza wakati wa uzinduzi huo, Waziri Silaa alisema mradi huo umekuja wakati mufaka haswa kutokana na ongezeko la uhitaji wa nyumba za makazi Jijini Dar es Salaam.
" Uamuzi wa kampuni hizi mbili wa kujenga nyumba za bei nafuu ni muhimu sana hapa nchini na ni mfano bora wa kuigwa na taasisi nyingine hapa nchini ili kukabiliana na changamoto inayohusiana na mahitaji ya nyumba bora za makazi”, alisema.
Waziri Silaa aliongeza kusema kuwa hatua zilizochukuliwa na makampuni hayo mawili zinaunga mkono juhudi za Serikali zinazolenga uweko wa nyumba bora za makazi na gharama nafuu kwa wananchi hapa nchini.
Naye Mkurugenzi wa Kanda wa Kampuni ya RE/MAX Coastal , James Prevost, alisema mradi wa Sky Royal haulengi uwekezaji wa nyumba za makazi tu, bali ni kielelezo cha uwekezaji wa nyumba nzuri na za uhakika ambao unalenga kutoa makazi mazuri na endelevu kwa wananchi na kwa bei nafuu.
“Ushirikiano wetu wa kampuni ya Coral Property Holdings hususan katika mradi huu wa Sky Royal, umetuwezesha kuwapatia wananchi Jijini Dar es Salaam maisha bora kupitia nyumba nzuri za makazi na zenye unafuu”alisema.
Mkurugenzi Mtendaji wa kampuni ya Coral property Holdings Li Jun, alisema mradi wa huu wa nyumba nafuu umelenga si kuwekeza kwenye nyumba tu, bali pia kuhakikisha wananchi wanakuwa na maisha endelevu, yenye ufanisi na ambayo yatachangia ustawi wa familia kwa ajili ya Watanzania.
“Uwekezaji huu umelenga kuunga mkono juhudi za Serikali zinazolenga kuhakikisha kunakuwa na nyumba nzuri za makazi na zenye bei nafuu; kupitia miradi ya maendeleo kama vile Sky Royal,”alisema.
© 2024 IPPMEDIA.COM. ALL RIGHTS RESERVED