Kesi ya Besigye kuondolewa Mahakama ya Kijeshi, mkewe atilia mashaka

By Mwandishi Wetu , Nipashe
Published at 11:49 AM Feb 17 2025
Kesi ya Besigye kuondolewa Mahakama ya Kijeshi, mkewe atilia mashaka.
Picha:Mtandao
Kesi ya Besigye kuondolewa Mahakama ya Kijeshi, mkewe atilia mashaka.

Serikali ya Uganda imetangaza kuwa itaiondoa kesi dhidi ya mpinzani mkongwe, Kizza Besigye, kutoka mahakama ya kijeshi na kuipeleka mahakama ya kiraia, huku ikimtaka asitishe mgomo wa kula gerezani.

Hata hivyo, ahadi hiyo imekataliwa na Winnie Byanyima, mke wa Besigye, ambaye pia ni Mkurugenzi Mtendaji wa shirika la UNAIDS, akisema kuwa hatua hiyo inatia mashaka.

Besigye, ambaye alikuwa mshirika wa zamani wa Rais Yoweri Museveni kabla ya kugeuka kuwa mpinzani wake wa muda mrefu, alianza mgomo wa kula mnamo Februari 10 kama njia ya kupinga kifungo chake.

Serikali ilikuwa imemtuhumu kwa uhaini kwa madai ya kutishia usalama wa taifa na ilikusudia kumshtaki katika mahakama ya kijeshi, licha ya Mahakama ya Juu kuamua kuwa hatua hiyo dhidi ya raia wa kawaida inakiuka katiba.

Hata hivyo, msemaji wa baraza la mawaziri na Waziri wa Habari, Chris Baryomunsi, amesema kuwa serikali sasa inaharakisha uhamishaji wa kesi hiyo hadi mahakama ya kiraia.

"Kama serikali, tunatekeleza uamuzi wa Mahakama ya Juu," alisema Baryomunsi alipokuwa akizungumza na shirika la habari la AFP.

Katika ujumbe wake wa awali kupitia mtandao wa X, waziri huyo alisema kuwa alitembelea Besigye gerezani Jumapili, akiwa pamoja na madaktari wake wa kibinafsi, na kumhimiza kusitisha mgomo wa kula wakati akisubiri uhamishaji wa kesi yake.