JKU, Chipukizi kibaruani Zanzibar

By Hawa Abdallah , Nipashe Jumapili
Published at 11:34 AM Sep 01 2024
JKU, Chipukizi kibaruani Zanzibar
Picha:Mtandao
JKU, Chipukizi kibaruani Zanzibar

MABINGWA wa Ligi Kuu Zanzibar, JKU wanatarajia kukutana na Chipukizi kutoka Pemba katika mechi ya Ngao ya Jamii itakayochezwa leo kwenye Uwanja wa Amaan Complex.

Mechi hiyo ni maalumu kwa ajili ya kufungua rasmi pazia la msimu mpya wa Ligi Kuu Zanzibar 2024/2025.

Akizungumza na gazeti hili jana, Kocha Mkuu wa Chipukizi, Mzee Ali, alisema wamejiandaa vyema kucheza soka la ushindani ili kuhakikisha wanabeba ngao hiyo.

Ali alisema ingawa mchezo huo sio rahisi kama unavyozaniwa lakini mipango yao mikubwa ipo kuhakikisha wanaanza msimu mpya kwa 'kishindo' kwa kucheza kwa tahadhari.

"Tumejiandaa kuhakikisha hatufanyi  makosa kuelekea mchezo huu muhimu wa ufunguzi wa ligi yaani Ngao ya Jamii, tunaamini kesho (leo) ni kupata ushindi na kuipata ngao ili kuwa na hamasa zaidi  kuelekea msimu mpya," kocha huyo alisema.

Naye Kocha wa JKU, Salum Haji, alisema licha ya kuwa na majeruhi watatu wa kikosi cha kwanza lakini anakikosi kipana kitakachotetea ngao hiyo.

"Tunashuka uwanjani kwenda kuitetea  ngao yetu ambayo mwaka jana tuliichukua na mwaka huu lengo kushinda kwa idadi  kubwa ya magoli," alitamba.