Gamondi aiona Yanga ikishinda ubingwa Afrika

By Faustine Feliciane , Nipashe Jumapili
Published at 10:18 AM Sep 22 2024
Wachezaji wa Yanga.
Picha: Mtandao
Wachezaji wa Yanga.

KOCHA wa Yanga, Miguel Gamondi amesema anaiona Yanga ikiwa karibu na kutwaa ubingwa wa Afrika kwa miaka ya karibuni kutokana na viwango vya wachezaji na uongozi mzuri walionao kwa sasa.

Akizungumza jana kabla ya mchezo wao wa marudiano wa hatua ya kwanza ya Ligi ya Mabingwa Afrika dhidi ya CBE ya Ethiopia, Gamondi, amesema kwa sasa Yanga ni moja ya timu kubwa na ya kuogopwa Afrika kutokana na uwezo wao.

"Kwa namna timu inavyoendeshwa na usajili unaofanyika kila dirisha la usajili linapofika naiona Yanga ikifanikiwa zaidi kwa miaka ya karibuni, ni timu yenye malengo, hii inatokana na aina ya uongozi walionao," alisema Gamondi.

Alisema mafanikio waliyoyapata katika misimu ya karibuni ni kielelezo tosha cha namna ya mwelekeo mzuri wa timu hiyo katika kufikia mafanikio waliyoyakusudia.

"Msimu uliopita tulikuwa na malengo ya kucheza hatua ya makundi, tulifanikiwa na kufikam paka robo fainali ya Ligi ya Mabingwa Afrika, lakini nyuma yake timu hii iliceza fainali ya Kombe la Shirikisho, hapo utaona ni timu inayopanda juu kwenye mafanikio ya Afrika," alisema Gamondi.

Gamondi akuacha kuizungumzia Ligi Kuu Tanzania Bara ambapo amesema ni ya ushindani na yenye msisimko mkubwa miongoni mwa Ligi za Afrika.

"Ligi hii inavutia wachezaji wengi kuja kucheza hapa, hii inatokana na ushindani wake na msisimko uliopo, mashabiki wake ni watu wanaooongeza chachu kwenye ligi, ndio maana unaona timu za Tanzania zinfanya vizuri zaidi ukilinganisha na timu nyingine za Afrika Mashariki kwenye mashindano ya CAF," alisema Gamondi.

 Mara baada ya mchezo wa jana usiku uliochezwa uwanja wa New Amaan Stadium, Yanga sasa inarejea kwenye michezo yake ya Ligi Kuu ambapo jumatatu inategemea kusafiri kuelekea Mbeya kwa ajili ya mikikimikiki ya Ligi hiyo.