Zitto: Kusuasua mradi wa Mchuchuma ni kuwakosesha vijana ajira

By Halfani Chusi , Nipashe Jumapili
Published at 01:18 PM Sep 15 2024

KIONGOZI Mstaafu wa Chama Cha ACT Wazalendo, Zitto Kabwe.
Picha: Mpigapicha Wetu
KIONGOZI Mstaafu wa Chama Cha ACT Wazalendo, Zitto Kabwe.

KIONGOZI Mstaafu wa Chama Cha ACT Wazalendo, Zitto Kabwe amesema kitendo cha serikali kusuasua kufanikisha Mradi wa Mchuchuma na Liganga ni makusudi wanawakosesha vijana ajira.

Zitto ameyasema hayo jana akiwa katika mwendelezo wa ziara mkoani Njombe baada ya kubaini hakuna kinachoendelea katika mradi huo.

Alisema alikuwa anausikia mradi huo unapigiwa kelele na wabunge wazamani na hata alipoingia bungeni alifanya hivyo lakini hakuna kilichobadilika.

Alisema katika kuhakikisha hilo linatimia yeye na aliyekuwa Mbunge wa Ludewa  Deo  Filikunjombe walipambana wakatafuta mwekezaji lakini hakufanikiwa kutokana na kile alichokiita kona kona za serikali.

Zitto alisema alishangaa kuona serikali inafurahia kulipa fidia ya Sh bilioni 15  kwa wakazi kupisha eneo hilo kwaajili ya uwekezaji wakati ilipaswa ifanye hivyo tangu miaka 10 iliyopita.

Alisema nchi inapoteza fedha nyingi kuagiza chuma nje ya nchi wakati chuma kipo kimelala Ludewa.

"Na mwenyezi Mungu anavyotupenda pembeni yake akaweka Makala ya Mawe ambayo yanatumika kuyeyusha chuma Ili kupata chuma cha pua lakini miaka yote hakuna kilichofanyika.

"Tunajenga reli tunajisifia, tunanua chuma kutoka China maana yake tumepeleka ajira kwenye nchi ya China wakati vijana wetu wapo mtaani wanahangaika na ajira" alisema Zitto 

Alikumbushia  mwaka Jana alipouwa Makambako alihoji serikali inapata kigugumizi gani kutekeleza mradi huo.

Alisema Ili kutengeneza msingi wa uchumi wa viwanda lazima tuwekeze Katika chuma akisisitiza hakuna uchumi wa viwanda bila bidhaa hiyo.

"Kitu Cha ajabu leo naambiwa na viongozi eti kiwanda cha kuongeza thamani kwenye chuma kitajengwa Makambako kwahiyo malighafi itatoka Ludewa kwenda huko uchumi wa wapi huu akili za kipuuzi kabisa.

"Chuma ni madude makubwa unayapelekaje huko kabla hayajapungua uzito hapa Ludewa? 

"Serikali iseme imebadilisha lini sera yake ya ujenzi wa reli kutoka Mtwara, Mbamba Bay, mpaka Ludewa kwenye mchuchuma na liganga?" Amehoji Zitto 

Amehitimisha mkutano wake kwa kuonya i kitendo cha serikali kuendelea na mpango wa kujenga kiwanda cha Chuma Makambako akisistiza ni uamuzi wa hovyo baadala yake akisisitiza kijengwe Ludewa.