|
Polisi watoza watumiaji barabara bila kutoa stakabadhi
2008-05-17 15:04:26
Na Radio One Habari
Polisi katika kituo cha Borega kilicho katika mpaka wa Tanzania na Kenya wilayani Tarime wanadaiwa kutoza kati ya shilingi elfu tano na elfu kumi kwa kila gari linalotumia barabara hiyo bila ya kutoa stakabadhi.
Baadhi ya wenye magari wameiambia Radio One Stereo kuwa magari mengi yanayotozwa fedha hizo ni ya huduma ya usafiri kwa wananchi wa vijijini na yasipotoa fedha hizo askari hao hukataa kufungua mlango wa kizuizi.
Wamedai kuwa mwezi mmoja uliopita akinamama wawili wajawazito kwa nyakati tofauti walijifungua ndani ya magari yaliyokuwa yakiwapeleka katika hospitali ya wilaya ya Tarime baada ya kukaa eneo hilo kwa zaidi ya saa nzima wakisubiri kuondolewa kwa kizuizi.
Hata hivyo meneja wa Mamlaka ya Mapato Tanzania -TRA mkoa wa Mara Bwana Leonard Shija amekanusha kuwa mamlaka hayo yanahusika na kizuizi hicho bali ni polisi kwani mamlaka yake ina ofisi eneo hilo ya kukusanyia ushuru.
Kamanda wa Polisi mkoa wa Mara Bwana DaviI Ole Saibullu naye amekanusha kuwa polisi inahusika na kizuizi hicho ni cha TRA.
|