|
Wizara ya Miundombinu kuendelea kutekeleza agizo la Rais mstaafu
2006-07-12 15:37:31
Na Radio One Habari
Wizara ya Miundombinu imelihakikishia bunge kwamba itaendelea kutekeleza agizo la Rais mstaafu wa awamu ya tatu, mheshimiwa Benjamin Mkapa kwa iliyokuwa Wizara ya Ujenzi katika serikali yake la kujenga barabara itakayopitika katika majira yote ya mwaka kuunganisha wilaya ya Simanjiro na mji wa Babati ambao ni makao makuu ya mkoa mpya wa Manyara.
Uthibitisho huo umetolewa bungeni mjini Ddodoma na Naibu Waziri wa wizara hiyo, mheshimiwa Makongoro Mahanga alipokuwa akijibu swali la Mbunge wa Simanjiro, mheshimiwa Christopher Ole Sendeka.
Amesema mpaka sasa shilingi Bilioni 1.4 zimeshatumika kwa ajili ya ujenzi wa sehemu ya barabara hiyo ambayo hadi itakapokamilika itagharimu kiasi cha shilingi Bilioni-18.
Mheshimiwa Mahanga amesema katika mwaka huu wa fedha barabara hiyo imetengewa kiasi cha shilingi Bilioni 1.35 na kwamba katika bajeti ya mwaka ujao wa fedha kiasi hicho kinatarajiwa kuongezeka.
Awali, mheshimiwa OLE Sendeka alionesha wasiwasi kwamba huenda barabara hiyo ikachukua zaidi ya miaka 20 kukamilika kutokana na kiasi kidogo cha fedha kinachotengwa kwa ajili hiyo kila mwaka.
|