|
Tume ya uchaguzi Kenya yatoa agizo kwa jeshi la polisi
2006-07-16 19:01:12
Na EAR Habari
Tume ya Uchaguzi nchini Kenya imeliagiza jeshi la polisi nchini humo, kuwakamata na kuwashitaki watumishi wa umma, wanaowapigia kampeni baadhi ya wagombea, katika uchaguzi mdogo unaotarajiwa kufanyika julai 24 mwaka huu.
Makamu Mwenyekiti wa Tume hiyo Gabriel Mukele, amesema kanuni za uendeshaji za uchaguzi zinaizuia serikali kutumia rasilimali za taifa kwa manufaa ya mgombea au chama chochote.
Amesema watumishi wa umma hawapaswi kushabikia upande wowote, hivyo tume hiyo itapambana vikali na mtumishi yeyote atakayekiuka sheria hiyo.
Uchaguzi huo mdogo utafanyika katika majimbo ya Nakuru Mjini, Laisamis, Horr Kaskazini, Saku na Moyale, kufuatia vifo vya wabunge watano, katika ajali ya ndege iliyotokea April 10 wilayani Marsabit.
|