|
Wanafunzi wa chuo cha Ustawi wapata rais wao
2008-05-13 17:48:36
Na Haji Mbaruku, Jijini
Mwandishi wa kujitegemea anayeandikia magazeti ya The Guardian, Bw.Dominic Nkolimwa, amechaguliwa kuwa Rais wa Serikali ya wanafunzi wa Chuo cha Ustawi wa Jamii kilichopo maeneo ya Kijitonyama, Jijini.
Bw. Nkolimwa anachukua nafasi ya Bw. Polycarp Benadict, ambaye amemaliza muda wake.
Hadi sasa, Bw. Nkolimwa tayari ameshaapishwa kubeba jahazi hilo la wanafunzi chuoni hapo ambao hivi karibuni ilikumbwa na matatizo mbalimbali na anatazamiwa kutangaza baraza la mawaziri wiki hii.
Bw.Nkolimwa ambaye ni mwanafunzi wa mwaka wa pili wa shahada ya rasilimali watu, amemshinda Bw.Francis Sunguya kwa kuzoa kura 369 kati ya kura 545, ambazo ni sawa na asilimia 68.
Bw. Francis ambaye pia ni mwanafunzi wa mwaka wa pili wa Sayansi ya Jamii, aameambulia kura 122 ambazo ni sawa na asilimia 22.
Akizungumza mara baada ya kushinda nafasi hiyo, Bw.Nkolimwa akasisitiza ahadi aliyokuwa akiitoa kuwa atashirikiana na wanafunzi wenzie chuoni hapo katika kutetea maslahi yao na pia kuimarisha ushirkiano wao na uongozi wa chuo ili hatimaye waweze kupata elimu bora.
Aidha, akaahidi kuimarisha Serikali yao ya wanachuo kwa kuhakikisha kuwa inakuwa na vifaa mbalimbali vya ofisi yao na hivyo kujihakikishia fursa ya kufanya kazi waliyotumwa na wanachuo wenzao kwa uhakika.
Pia akaahidi kushirikiana na viongozi wenzie katika kuhakikisha kuwa chuo kinahuisha mtandao wake ili wanafunzi wapate matokeo ya mitihani yao kupitia njia hiyo.
Kuhusiana na migomo ya mara kwa mara inayofanywa na wanafunzi wa vyuo vya elimu ya juu, Bw. Nkolimwa akaahidi kushirikiana na menejimenti ya chuo katika kuhakikisha kuwa migomo hiyo inapatiwa ufumbuzi wa kudumu, ikiwemo ile ya kuhakikisha kuwa wanakuwa na mawasiliano mazuri na Bodi ya Mikopo ya wanafunzi ili wale wote wanaostahili waweze kupata mikopo hiyo kwa wakati muafaka.
|