|
Msichana wa kazi Dar afariki kwa umeme
2008-05-07 19:43:39
Na Kiyao Hoza, Polisi Kati
Mfanyakzi wa ndani aitwaye Lydia Batholomeo,16, amefariki dunia baada ya kupigwa na shoti ya umeme wakati akiosha vyombo.
Kamanda wa Mkoa wa kipolisi Kinondoni, Jamal Rwambow, amesema tukio hilo limetokea mishale ya saa 11:00 jioni katika eneo la Tegeta Jijini.
Akasema eneo alilokuwa akiosha mfanyakazi huyo wa ndani lilikuwa na waya wa umeme uliochubuka.
Akasema wakati akiendelea na shughuli yake hiyo, alimwaga maji katika eneo hilo na kisha kuyakanyaga na hivyo akapigwa shoti na kufariki dunia.
Akasema msichana huyo alikuwa akiishi katika nyumba ya Bw. Mathayo Lema.
Wakati huo huo, mkazi wa Goba Jijini aitwaye Augustino Ngowi ,60, amefariki dunia baada ya kugongwa na gari.
Akasema ajali hiyo ilitokea jana, mishale ya saa 1:20 usiku katika barabara ya kuelekea kiwanda cha kutengeneza soda cha Coca Cola.
Akalitaja gari lilomgonga mzee huyo kuwa ni Toyota Coaster, lenye namba za usajili T 306 AHV, ambalo lilikuwa likitokea Mwenge kuelekea Coca Cola.
Hata hivyo, Kamanda Rwambow amesema kuwa dereva wa gari hilo alikimbia baada ya kutokea kwa ajali hiyo na hadi sasa anasakwa na Polisi.
Akasema miili ya marehemu wote imehifadhiwa katika chumba cha kuhifadhia maiti cha Hospitali ya Mwananyamala.
|