|
Majambazi yajifanya abiria na kupora teksi
2008-05-05 18:29:54
Na Kiyao Hoza, Polisi Kati
Watu wawili wanaosadikiwa kuwa ni majambazi wamempora gari dereva teksi huko Kigamboni eneo la South Beach.
Kamanda wa Mkoa wa Kipolisi wa Temeke, Emmanuel Kandihabi, amesema tukio hilo limetokea jana mishale ya saa 2:00 usiku katika eneo hilo la South Beach.
Kamanda Kandihabi amesema, kwa mujibu wa maelezo ya dereva teksi huyo, Abdalah Ahmed, 31, aliyekuwa akiendesha gari namba T 105 AKY Toyota Corolla inayoegeshwa maeneo ya Ubungo, jirani na tawi la benki ya NBC .
Amesema akiwa katika eneo la kazi alikodiwa na mtu mmoja akimtaka ampeleke huko South Beach Kigamboni.
Amesema kabla ya kuondoka aliwasiliana na mtu mwingine ambapo walikubaliana amkute njia panda ya Mji Mwema.
Ameendelea kusema kuwa walipofika katika eneo hilo, walimkuta mtu huyo ambaye ni mwanaume na kumchukua ambapo waliendelea na safari yao hadi eneo hilo la South Beach.
Kamanda Kandihabi amesema ghafla abiria laiyekuwa ameketi kiti cha mbele alishuka katika gari na aliyekuwa kiti cha nyuma, alimfunga kamba ya mdomo dereva huyo na kisha kumvuta hadi katika kiti cha nyuma.
Amesema baadaye watu hao walimpekua na kumpora kiasi cha Sh. 30,000 alizokuwa nazo pamoja na simu aina ya Nokia.
|