|
Mume Dar alizwa gari huku mkewe akishuhudia
2008-05-05 18:26:24
Na Kiyao Hoza, Polisi Kati
Watu wanne waliokuwa na bastola na silaha nyinginezo wamemshusha ndani ya gari mwanamke mmoja na kisha kupora gari la mumewe na kutokomea nalo kusikojulikana.
Kamanda wa Mkoa wa Kipolisi Ilala, Faustine Shilogile, amesema tukio hilo limetokea jana majira ya saa 2:00 asubuhi katika maeneo ya Kariakoo Jijini.
Kamanda Shilogile amesema Polisi walipata taarifa toka kwa Bw. Ahmed Alawi, 43, aliyedai kuwa akiwa na gari lake lenye namba T171 ASS, aina ya Toyota Mark II pamoja na mkewe Bi. Sabrina, walifika kwenye duka moja la mfanyabiashara aliyejulikana kwa jina la Bw. Kani ili wafanye manunuzi ya vitu mbalimbali.
Amesema walipofika dukani hapo, akamuacha mkewe ndani ya gari na kuingia dukani.
Akasema mara, wakati yeye Ahmed akiwa dukani, wakafika majambazi wanne wakiwa na bastola na kumtaka mkewe ashuke ndani ya gari hilo, lakini akakaidi.
Hata hivyo, akasema majambazi hao walifanikiwa kumtoa kwa nguvu ndani ya gari hilo kabla ya kwenda nalo kusikojulikana.
Kamanda Shilogile amesema hakuna anayeshikiliwa kufuatia tukio hilo.
Hata hivyo, akasema Polisi wanaendelea kuwasaka majambazi hao ili kuwatia mbaroni.
|