|
Serikali yaahidi kuzisaidia SACCOS
2008-02-27 17:22:15
Na Valery Kiyungu, Tegeta
Serikali imeahidi kuelekeza nguvu zake katika Vyama vya akiba na mikopo, SACCOS, kwa kusaidia kutoa wataalam zaidi ili kuviwezesha kufanya kazi vizuri na hatimaye kutimiza malengo ya kuanzishwa kwake.
Aidha, Serikali imeechukua jukumu hilo la kuvisaidia vyama hivyo kwa vile ni miongoni mwa njia za kuwawezesha Watanzania na hatimaye kujikwamua kiuchumi.
Hayo yamesemwa na Afisa Maendeleo ya Vijana Mwandamizi, Wizara ya Kazi, Ajira na Maendeleo ya Vijana, Bw. Julius Tweneshe, wakati alipokuwa akizinduua chama cha akiba na mikopo cha nyuki, Nyuki SACCOS, kilichopo Tegeta nje kidogo ya Jiji la Dar.
Bw. Tweneshe amesema Serikali, kupitia wizara yake, imejipanga vyema kuzisaidia SACCOS, kwa kuhakikisha kuwa wanachama wa vyama hivyo wananufaika kwa kupata mikopo yenye masharti nafuu.
``Serikali kupitia Wizara ya Kazi Ajira na Maendeleo ya Vijana nchini itazisaidia SACCOS ili kuviwezesha vyama hivyo kuendelea kuhudumia wanachama wake kwa ukamilifu,`` akasema Bw. Tweneshe.
Aidha, afisa huyo akasema ofisi yake imeweka mlango wazi kwa vyama hivyo, ambapo amewataka viongozi wao kufika ofisini kwake pindi wanapohitaji ushauri wa kitaalam.
Wakarti wa kuwasilisha taarifa yao, Nyuki SACCOS walidai kuwa wana wanachama 70 ambao ni wafanyabiashara wa Soko la Nyuki na pia, wanachama wengine ni wakazi wa maeneo mbalimbali na ya Jiji ambao wametimiza masharti ya kujiunga na chama hicho.
|