|
Vijana wa `vijiweni` Tandale kuelimishwa kuhusu ukimwi
2008-02-27 17:21:05
Na Jacqueline Mosha, Jijini
Vijana 34 wanaowakilisha vikundi 12 vya kambi kutoka kwenye mitaa mbalimbali ya Kata ya Tandale Jijini wako katika mafunzo ya wiki mbili kwa ajili ya kujifunza elimu rika, malezi ya ujana na afya ya uzazi.
Katibu wa asasi isiyo ya kiserikali ya LUMBESA, Bw. Lumona Kibore, amesema mradi huo wa mafunzo unaofadhiliwa na Family Health International ni wa miezi mitatu, ukilenga kuelimisha vijana wa kempu mbalimbali.
Bw. Kibore akabainisha kuwa, mafunzo hayo yanayowahusisha vijana walio katika umri wa miaka kati ya 15 - 24 wa jinsia zote, yanalenga pia kuwapa uwezo vijana hao ili baadaye waweze kurejea kwenye kambi zao na kutoa elimu hiyo kwa wenzao, hasa kuhusu afya ya uzazi, stadi za kazi na ukimwi.
``Kabla ya kuandaa mafunzo haya, tulifanya utafiti na kugundua kuwa vijana wengi hawana uelewa kuhusu wa kutosha kuhusu ukimwi na mabadiliko ya tabia... ndio maana tukaandaa programu hii,`` akasema Bw. Kibore.
Baadhi ya vijana watakaofadikika na mafunzo hayo ni pamoja na wale wa kambi za Wagiriki, Mangilimaa, Mafyonso, Ubalozi na Mabahasha.
Wengine ni wa kambi za Nyangumi, The Kingdom, Kitofa, Niggas Nature, Liverpool, Misosi Billionaire na Wapalianda.
|