|
Anaswa Airport Dar na madawa
2007-05-02 18:05:56
Na Sharon Sauwa, Jijini
Mkazi mmoja wa Mabawa mkoani Tanga amenaswa na madawa ya kulevya aina ya Heroin pale katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere Jijini wakati akiwasili kutoka nchini India.
Mtu huyo, aliyetajwa kwa jina la Mtemi Kwimba, amenaswa na pipi 27 za madawa hayo haramu.
Kamanda wa kikosi cha Madawa ya Kulevya Nchini, Bw. Nzowa, ameiambia Alasiri leo asubuhi kuwa mtu huyo alidakwa na polisi saa 10.00 jioni Aprili 29 mwaka huu.
Kamanda Nzowa akasema, mtuhumiwa alikamatwa uwanja wa ndege wakati akitua na dege moja lililotoka nchini India.
Akasema kukamatwa kwa mtu huyo kulifuatia kushukiwa kuwa alikuwa amebeba madawa hayo ya kulevya.
``Askari walimshuku na kumkamata… alipohojiwa akakubali kuwa amemeza pipi za madawa hayo haramu,`` akasema Kamanda Nzowa.
Akieleza zaidi, Kamanda Nzowa akasema mtuhumiwa huyo aliondoka nchini Machi 7 mwaka huu akitokea Tanga.
Akasema baada ya hapo, safari ya mtuhumiwa ikaanza kwa kupitia Hororo, akatua Nairobi nchini Kenya, akaenda Dubai na hatimaye akafika huko India.
Hata hivyo, akasema thamani ya madawa hayo bado haijafahamika na kwamba mtuhumiwa anatarajiwa kufikishwa mahakamani kesho.
|