|
Baiskeli yaua mtu Dar
2007-05-02 18:04:23
Na Kiyao Hoza, Polisi Kati
Katika hali ya kushangaza, mkazi mmoja wa Msimbazi Centre Jijini Dar es Salaam, Waziri Said, 57, amefariki dunia baada ya kugongwa na baiskeli.
Kamanda wa mkoa wa kipolisi wa Ilala, Masindoki Masindoki, amesema tukio hilo lilitokea jana saa 4.30 asubuhi huko Maguruwe, Kigogo.
Amesema Said aligongwa na baiskeli iliyokuwa ikiendeshwa na Godfrey Pius, 20 ikitokea barabara ya Kawawa kuelekea Kigogo, Mbuyuni.
Kamanda Masindoki amesema mtu huyo alifariki dunia wakati akipelekwa katika Hospitali ya Amana kwa matibabu.
Aidha amesema polisi wanamsaka mwendesha baiskeli huyo aliyetoweka baada ya ajali.
Wakati huohuo, watu tisa wanashikiliwa na polisi kwa kupatikana na banghi gramu 60 na misokoto 35.
Kamanda Masindoki amesema tukio la kwanza lilitokea saa 6.00 mchana huko Vingunguti ambapo watu wanne walidakwa na madawa hayo.
Amewataja watuhumiwa hao kuwa ni Juma Mohamed, 20, Yasin Mohamed, 22, Ramadhan Mohamed, 27 na Athuman Ally, 22.
Tukio la pili amesema lilitokea saa 3:00 asubuhi jana katika eneo la Magomeni Jangwani ambapo watu watano walikamatwa na madawa hayo.
Kamanda wa mkoa wa kipolisi wa Kinondoni, Jamal Rwambow amewataja waliokamatwa kuwa ni Badru Hamis, 24, Bakari Ally, 22, Rishard Born, 25, Deo Mropo, 20 na Abuu Mohamed,30.
|