|
Mavuno yameanza lakini bei ya chakula haishuki
2006-07-24 15:33:03
Na Claudia Kayombo, Ukonga
Baadhi ya wakazi wa kata ya Ukonga wameiomba Serikali kuingilia kati bei kubwa ya vyakula ambayo ni tishio kwa wakazi wa eneo hilo hasa wenye kipato cha chini.
Wakizungumza na gazeti hili baadhi ya wakazi wa kata hiyo wamesema pamoja na kipindi hiki kuwa ni cha mavuno bado bei ya vyakula inatishia maisha ya walaji hasa wale wenye kipato cha chini.
Wamesema tofauti na miaka mingine ambapo kipindi cha mavuno cha kati ya miezi ya Juni na Septemba bei ya vyakula ilikuwa inashuka kwa zaidi ya asilimia 50, mwaka huu hali imekuwa kinyume chake.
Tunachofahamu sisi miaka yote kipindi cha mavuno bei ya vyakula inapungua kwa kiasi kikubwa lakini mwaka huu bei imendelea kuwa juu kama mwanzo, amesema Joseph Fransis mkazi wa Ukonga, Mombasa.
Wakazi hao wamezidi kuiomba Serikali kuwakoromea wafanyabiashara na wachuuzi ili wasiendelee kuwanyonga wananchi kwa tamaa ya kujipatia pesa za haraka haraka.
Gazeti hili pia limeshuhudia katika masoko ya Gongo la mboto na Guluka Kwalala ya kata hiyo bei za vyakula zikiwa kubwa kama ilivyokuwa kabla ya kipindi cha mavuno kuanza.
Katika masoko hayo Alasiri imeshuhudia mchele ukiuzwa kwa kati ya Sh. 1100 na 800 kwa kilo, maharage kati ya Sh. 1100 na 700, na unga Sh. 550 na 460.
Wamesema kipindi kingine cha mavuno mchele ulikuwa hauzidi Sh. 600 wa kilo, unga Sh. 300 na maharage Sh.600.
|