|
Chonde chonde JK na sisi tuongeze posho, Wazee wa Baraza wasema
2006-07-19 14:45:35
Na Hakhi Yunga,Jijini
Wazee wa Baraza katika mahakama za Mwanzo Jijini, wamemuomba Rais Jakaya Mrisho Kikwete na Waziri wa Sheria na Katiba Bi.Mary Nagu walivalie njuga suala la nyongeza ya posho waliyoiomba kwani kiasi cha Sh.1500 wanacholipwa kwa sasa ni kidogo.
Aidha, wazee hao wametoa pongezi zao za dhati kwa Rais Kikwete pamoja na Waziri wa Sheria na Katiba Bi.Mary Nagu kwa jitihada walizozifanya za kulitafutia ufumbuzi tatizo la kucheleweshwa kwa posho zao, hali iliyosababisha kulipwa kwa wakati unaotakiwa yaani kila mwezi.
Hayo yamesemwa na Wazee wa Baraza wa Mahakama ya Mwanzo Kinondoni kwa niaba ya wenzao wakati wanaongea na gazeti hili.
Wamesema awali walikuwa wakilipwa posho zao baada ya miezi mitano hadi sita lakini walipoamua kutoa kilio hicho, kwa Msajili wa Mahakama Kuu ya Rufaa, Rais Kikwete akaingilia kati na tatizo hilo kupatia ufumbuzi.
Wamesema kiasi cha Sh.1500 wanacholipwa kwa sasa ni kidogo sana na hakitoshelezi kukidhi mahitaji yao ya kila siku kutokana na gharama za maisha kuwa juu.
|