|
DAWASCO sasa kutumia kompyuta kuwabana vishoka
2006-07-07 16:35:23
Na Emmanuel Lengwa, Sabasaba
Kampuni ya usambazaji maji safi na maji taka Dar es Salaam, DAWASCO, imeanzisha mpango mpya wa kukusanya ankara zake kwa lengo la kudhibiti watu waliokuwa wakihujumu mapato ya kampuni hiyo maarufu kama vishoka.
Chini ya mpango huo, stakabadhi zote za zamani zimetupiliwa mbali na badala yake zitatumika stakabadhi mpya ambazo zimeunganishwa na akaunti ya mteja kwa kutumia programu maalum ya kompyuta.
Stakabadhi hizo mpya zitaonyesha kila aina ya malipo yanayofanywa na mteja kwa wakati pamoja na maelezo mengine muhimu yanayohusu akaunti ya mteja husika.
Mpango huo ulitangazwa jana na Mkurugenzi wa DAWASCO, Bw.Alex Kaaya wakati akizungumza na waandishi wa habari ndani ya banda la kampuni hiyo kwenye maonyesho ya Sabasaba yanayoendelea kwenye viwanja vya Mwalimu Nyerere, Barabara ya Kilwa jijini Dar es Salaam.
Bw.Kaaya amesema mpango huo utaanza kutumika rasmi katika ofisi zote za kukusanyia malipo Jijini.
Amesema mpango huo utamaliza malalamiko ya muda mrefu ya wateja kudai kubambikiwa bili na wale waliokuwa wakilalamika kuwa wamelipa lakini malipo hayaonekani na badala yake kuendelea kudaiwa.
Bw.Kaaya amesema kampuni yake imekuwa ikikabiliwa na matatizo makubwa mawili ambayo ameyataja kuwa ni ankara za wateja kuonyesha matumizi ya uongo na lile la upungufu wa maji kwa wakazi wa Jiji.
Natoa wito kwa wateja waliokatiwa maji kufika ofisi za Dawasco kujieleza ili matatizo yao yatatuliwe, akasema Bw. Kaaya.
Hata hivyo, amesisitiza kuwa mpango huo haujakusudia kufuta madeni ya wadaiwa sugu.
|