



Waziri wa Fedha Dk. William Mgimwa, amesema sensa ya Agosti mwaka huu ndicho kipimo kitakachotumika kupima mafanikio ya Tanzania kwenye kutekeleza Malengo ya Milenia (MDGs) ya Umoja wa Mataifa.
Dk. Mgimwa alisema hayo wakati wa ufunguzi wa mafunzo ya wakufunzi wa sensa ngazi ya taifa kutoka Bara na Visiwani yaliyoanza juzi mjini Dodoma na kuongeza kuwa itatoa viasharia iwapo Tanzania imetimiza MDGs ifikapo 2015.
Malengo hayo ni pamoja kuondoa umaskini kwa asilimia 50, kupunguza vifo vya wazazi na watoto wachanga, kumaliza njaa, kuleta usawa wa kijinsia, kudhibiti maambukizi ya VVU na kutunza mazingira.
Alisema takwimu hizo pamoja na kuwezesha kujulikana idadi kamili ya watu, elimu, ndoa, umri, vifo, vizazi na ajira zitawezesha kutathmini hali na ubora wa maisha ya wananchi na kupanga mikakati ya maendeleo endelevu.
Waziri Mkuu , Mizengo Pinda, akifungua mafunzo hayo, alisisitiza kuwa kutokana na umuhimu wa sensa kwa maendeleo ya taifa ni lazima viongozi wote wa dini, siasa na asasi za kiraia watoe ushirikano wa dhati ili kufanikisha zoezi hilo.
Pinda, amewataka viongozi wote kuhamasisha na kuelimisha umma kuhusu umuhimu wa sensa ya watu na makazi na kuhakikisha kuwa Watanzania wanashiriki na kutoa taarifa sahihi.
Aidha aliwataka Watanzania kutunza kumbukumbu za taarifa za maswali yatakayo ulizwa kwa watu wote watakaokuwa wame lala kwenye kaya usiku wa kuamkia Agosti 26, mwaka huu ambayo ndiyo siku ya sensa.